Kwa Kiswahili hufahamika zaidi kama maambukizi ya sehemu ya juu ya mfumo wa uzazi wa mwanamke ikihusisha mlango wa kizazi, mji wa uzazi, mirija ya uzazi pamoja na vifuko vya mayai ya uzazi.
PID hutokea baada ya kupanda juu kwa bakteria wabaya kutoka kwenye uke na mlango wa kizazi kwenda kwenye kuta za mji wa uzazi na mirija ya uzazi.
Uambukizwaji
Neisseria gonorrhoeae, Chlamydia trachomatis na Mycoplasma genitalium ndiyo vijidudu hatari zaidi kwa kusababisha PID, na husambazwa kutoka mtu mmoja kwenda mwingine kwa njia ya ngono, hivyo uwepo wa magonjwa ya zinaa hasa Kisonono na Klamidia huchangia kwa kiasi kikubwa kutokea kwa ugonjwa wa PID.
Mtu anaweza pia kupata ugonjwa huu kutokana na uwepo wa maambukizi makali baada ya kutoa ujauzito, kuharibika kwa ujauzito au baada ya kufanyika kwa utaratibu wowote ule unaofungua tumbo.
Katika hali chache, bakteria wazuri wanaopatikana kwenye uke wanaweza kugeuka wabaya ikiwa watavuka mlango kwa kizazi na kuingia sehemu ya juu ya viungo vingine.
PID inaweza kusababisha ugumba, utasa, maumivu ya kudumu ya tumbo la chini na nyonga pamoja na kuvurugika kwa mzunguko wa hedhi.
Ni vizuri ikishughulikiwa vizuri, mapema na kwa usahihi.
Dalili
Dalili za ugonjwa huu hutofautiana kulingana na hatua husika. Sio kila mwanamke huonesha dalili za kufanana na mwingine.
Pamoja na uwepo wa tofauti hizi, dalili za ujumla za ugonjwa huu ni;
Maumivu makali sehemu ya chini ya tumbo
Homa kali
Kutokwa na damu katikati ya mzunguko wa hedhi
Mlango wa kizazi huwa mwekundu sana, ambao mara nyingi hutoa uchafu mzito wenye rangi ya njano-kijani
Kuvurugika kwa mzunguko wa hedhi
Baadhi ya wanawake huwa hawaoneshi dalili kubwa, na hudhani kuwa wapo sawa kabisa. Changamoto huja wakati wa kutafuta ujauzito, wengi hushitushwa na ugumu katika kufanikisha zoezi hili.
Maumivu wakati wa haja ndogo na wakati wa tendo la ndoa
Tiba
PID inaweza kutibiwa kwa kutumia madawa (viua vijasumu-antibiotics) mfano Azithromycin, Ceftriaxone, Clindamycin, Gentamicin na Doxycyline.
Mhudumu wa afya atakuelekeza matumizi sahihi ya dawa pamoja na dozi sahihi kwa kadri atakavyoona inafaa.
Kinga
Njia za kujikinga na ugonjwa huu zipo wazi. Unaweza kujikinga kwa kufanya mambo yafuatayo;
Kuwa mwaminifu, tulia na mpenzi mmoja.
Wakati wa matibabu, ni vizuri ukijizuia wewe na mwenzi wako kushiriki tendo la ndoa ili kuepuka nafasi ya kuambukizana tena. Inafaa msubiri hadi ugonjwa upone.
Ili kukata mnyororo wa maambukizi, ni vizuri wapenzi wote wakitibiwa kwa pamoja. Ni muhimu kukumbuka kuwa,wanaume hawawezi kuugua PID lakini huwa na uwezo wa kubeba bakteria wanaosababisha tatizo hili na kuwapitisha kwa mwanamke wakati wa tendo la ndoa.
Muhtasari
Ni muhimu pia mwanamme akienda hospitalini kuchunguzwa pamoja na mwanamke kwani anaweza kuwa chanzo cha ugonjwa huu. (6)
Aidha, siyo kila uchafu mweupe, manjano au kijani unaotoka ukeni humaanisha PID, pia siyo kila maumivu yanayotokea chini ya tumbo, kutokwa na damu au hata uwepo wa maumivu makali wakati wa tendo la ndoa huwa wa PID.
Epuka kununua vitu dukani, mitandaoni au mtaani bila kupima kwanza hospitalini, utaumia.
Mvurugiko wa homoni (Hormonal imbalance)
Homoni au kwa lugha nyingine zikifahamika kama vichocheo vya mwili, ndiyo kemikali zinazosambaza taarifa za mwili kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine.
Taarifa hizi huviamuru viungo mbalimbali vya mwili nini cha kufanya na kwa wakati gani.
Tunaposema kuwa unasumbuliwa na tatizo la mvurugiko wa homoni (hormonal imbalance) huwa tunamaanisha kuwa, homoni fulani mwilini mwako zipo nyingi sana, au chache sana kulinganisha na kiwango sahihi kinachopaswa kuwepo.
Mabadiliko madogo ya kiwango cha homoni kinachopaswa kuwepo mwilini kinaweza kusababisha matatizo makubwa kwenye afya ya mhusika, pamoja na utaratibu wa kawaida wa maisha yake ya kila siku. (2, 3)
Chanzo
Kuna mambo mengi yanayoweza kusimama kama chanzo cha kuvurugika kwa homoni.
Kwa kuwa mwili wa binadamu huwa na homoni nyingi zinazozalishwa na tezi tofauti tofauti, sababu au vyanzo vya tatizo hili hutofautiana pia.
Miongoni mwake ni;
Matumizi ya baadhi ya madawa, mfano bangi
Matibabu ya saratani
Uvimbe kwenye tezi za pituitary
Mkazo (stress)
Ajali
Magonjwa hasa ya kisukari na yale yanayohusisha tezi za thyroid
Umri wa ukomo wa hedhi
Ujauzito na unyonyeshaji
Matumizi ya njia za uzazi wa mpango mfano kitanzi, majira, vijiti au sindano za depo provera.
Uzito uliozidi pamoja na mtindo mbaya wa maisha hasa upande wa mlo na vinywaji
Dalili
Dalili za uwepo wa tatizo hili hutofautiana kulingana na aina ya homoni inayosumbua, sehemu ambayo homoni husika hufanya kazi pamoja na jinsia ya mhusika.
Kwa ujumla wake, tatizo hili huwa na dalili zifuatazo
Mvurugio wa mzunguko wa hedhi unaoweza kusababisha hedhi ije kubwa sana, hedhi isionekane kwa miezi kadhaa, hedhi ipotee kabisa au pia ije bila kufuata utaratibu maalum huku ikiambatana na maumivu makali sana.
Kusumbuliwa na matatizo ya usingizi
Chunusi nyingi
Uchovu bila sababu
Kupoteza kumbukumbu haraka
Kichefuchefu, kuharisha pamoja na maumivu ya tumbo yanayotokea bila mpangilio maalumu
Kupoteza hamu ya kula
Ongezeka la ghafla la uzito wa mwili bila sababu maalum
Uke kuwa mkavu pamoja na kupungua au hata kuisha kabisa kwa hamu ya kushiriki tendo la ndoa
Kutokwa sana na jasho kila mara
Msongo wa mawazo
Ugumba
Kuota kwa ndevu pamoja na nywele kwenye sehemu mbalimbali za mwili (Wanawake)
Maumivu makali wakati wa tendo la ndoa
Kwa wanaume, huwa na dalili ya ziada ya kupunguza hamu na ufanisi kwenye kushiriki tendo la ndoa
Tiba
Mhudumu wako wa afya atauliza maswali kadhaa hivyo ushirikiano wa kutosha unapaswa kutolewa.
Ikiwa ataona inafaa, vipimo vitachukuliwa ili kubaini homoni zinazosumbua kwa wakati huo.
Utaratibu wa aina ya matibabu, dawa pamoja na dozi utategemea na homoni zenyewe, ukubwa wa tatizo na athari zilizopo kwa wakati huo.
Ikiwa homoni zako zitakuwa ni chache, matibabu makuu ni kupewa dawa zenye kuweka sawa homoni hizo, utaratibu ambao kitaalam huitwa Hormone Replacement Therapy ambayo inaweza kufanyika kwa njia ya sindano au vidonge.
Kwa watu wenye homoni nyingi kuliko kiwango cha kawaida, baadhi ya dawa zinaweza kutumika, upasuaji, tiba ya mionzi au mjumuiko wa njia zote unaweza kufanyika.
Baadhi ya dawa zinazoweza kutumika ni Metformin, Levothyroxine na Clomiphene citrate.
Kinga
Mvurugiko wa homoni unaweza kuwa na madhara hasi kwa afya ikiwa hautatibiwa haraka.
Kwa kuwa tatizo hili limekuwa kubwa sana siku hizi kutokana na athari za aina ya maisha tunayoishi, ni muhimu kufanya uchunguzi wa mara kwa mara ili kubaini kama lipo, ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa.
Baadhi ya mambo yanayoweza kufanyika ili kujikinga na tatizo hili ni;
Kutunza uziti sahihi wa mwili
Kula mlo bora
Kufanya mazoezi ya mwili
Kudhibiti stress pamoja na kupata muda mwingi wa kupumzika
Kufuatilia tiba sahihi ikiwa unaugua magonjwa sugu
Acha kuvuta sigaara
Tatizo hili hukaribisha magonjwa sugu, pamoja na kudumaza ubora wa afya ya uzazi kwa ujumla wake.
Muhtasari
Kama unapatwa na dalili usizozielewa ni muhimu kufika hospitalini ili upats uchunguzi na tiba. Kwa kuwa homoni za mwili ni balozi mwema anayetoa taarifa mbalimbali zenye kuupa amri mwili wako, ni lazima uhakikishe zipo sawa kila muda.

